Matini Muhimu :
Home » » AMRI ABEDI KALUTA (MSHAIRI GWIJI)

AMRI ABEDI KALUTA (MSHAIRI GWIJI)

Imeandikwa na; Unknown mnamo, Jumapili, 29 Desemba 2013 | Jumapili, Desemba 29, 2013




1.0        Historia ya Sheikh Kaluta Amri Abedi

 Sheikh Kaluta Amri Abedi alizaliwa Ujiji Kigoma mnamo mwaka 1924 Baba yake Kaluta Amri Abedi aliitwa Abedi bin Kaluta. Kaluta Amri Abedi Alikuwa ni mtoto wa pili wa kiume katika familia ya watoto kumi. Sheikh Kaluta Amri Abedi alipofika umri wa miaka 6 hivi alianza masomo ya Kurani mwaka 1930. Baada ya miaka mitatu ya masomo ya kurani  aliingia katika  shule ya masomo ya Kizungu. Baada ya kumaliza elimu ya awali mwaka 1937 alijiunga na Shule ya Sekondari Tabora.Baada ya masomo yake ya sekondari Sheikh Kaluta Amri Abed alikwenda kusomea ukarani wa posta Dar-es-salaam 1942—1943 .Kaluta Amri Abed alikwenda kusoma elimu ya dini Rabwah Pakistan ambako aliweza kufaulu vizuri na kuweza kutunukiwa shahada ya elimu ya dini (Teolojia).
Sheikh.Kaluta Amri Abedi alioa mke wake wa kwanza 1941 ambaye aliitwa Zamda bint Sudi ambaye alibahatika kuwa na mtoto mmoja aliye itwa Radhia kabla ya kumtaliki kutokana na upinzani mkubwa uliotokana na mgogoro wa tofauti za kidhehebu yaani Kaluta alipo hamia madhehebu la Ahamadiyya tofauti na mke ambaye alitoka katika familia yenye imani ya madhehebu ya sunni. Sheikh Kaluta Amri Abedi alioa mke mwingine mwaka 1956 ambaye aliitwa Amina bint Hamisi Mlenzi ambaye alibahatika kuzaa naye watoto sita na kufanya jumla  ya watoto saba
Sheikh Kaluta katika maisha yake amekuwa mtumishi wa serikali kwa nyadhifa mbalimbali,kama: aliwahi kuwa Mbunge wa kigoma, aliwahi kuwa meya wa kwanza mwafrika wa jiji la kwanza Dar-es-salaam, aliwahi kuwa mkuu wa mkoa jimbo la Magharibi,aliwahi kuwa waziri wa sheria,mpaka mauti yanamkuta alikuwa waziri wa maendeleo na utamaduni.
Katika dini Sheikh Kaluta alikuwa  Sheikh na mbashiri katika imani ya kiislam ya Ahamadiyya  alijishughulisha na  kueneza dini pamoja na kutafsiri  kurani katika lugha ya Kiswahili na lugha za kizungu.
Sheikh Kaluta Amri Abedi alikuwa na kipaji cha usanii. Kipaji hiki cha usanii kilianza kuonekana alipofika umri wa miaka 13, aliweza kutunga na kuimba  mashairi kwa  sauti nzuri na pia aliweza kudhibiti kanuni za mizani. Aliweza kusoma mashairi ya lugha ya Kiingereza, Kiurdu, Kiarabu na kiajemi.


         2.0      Mchango wa Kaluta Amri Abedi kwenye lugha ya kiswahili
Katika  maandishi ya Mathias Eugen Mnyampala yanayotaja historia ya maisha ya:
Sheikh Kaluta Amri Abedi, Mwandishi Mathias Eugen Mnyampala amemtaja Kaluta kama mtu hodari wa kutumia Lugha ya Kiswahili katika fani ya kuimba Tajuwidi, Mashairi na Tenzi kwa mahadhi ya namna mbalimbaali za Maghani.  Hivyo Mnyampala anaweka bayana mchango mkubwa wa Sheikh Kaluta Amri Abedi kwenye Lugha ya Kiswahili kama ifuatavyo:

          2.1 Kaluta Amri Abedi akiwa na umri wa miaka sita
 Kaluta Amri Abedi alionyesha dhamira ya kupenda Lugha ya Kiswahili, alianza kupigania matumizi ya Lugha ya Kiswahili tangu akiwa na umri mdogo kati ya miaka sita, ambapo akiwa mwanafunzi wa masomo ya Kurani alionyesha kutoridhika kujifunza Kurani kwa Lugha ya Kiarabu tu hata akadiriki kumuuliza mwalimu wake Kwa nini tunasoma kama kasuku hatuelewi yaliyomo katika aya za kurani tukufu?  Kwa nini kurani haitafisiriwi katika Lugha ya Kiswahili.”  Hata waalimu wake walipomjibu juu ya maneno ya Kiarabu kuonyesha ukamilifu wa aya na madai ya Masheikh wake kwamba kurani ikitafsiriwa ingeharibiwa maana yake tofauti na zilivyoteremshwa na Mwenyezi Mungu, Kaluta Amri Abedi hakuridhika na majibu hayo aliendeleza jitihada za kudai matumizi ya Lugha ya Kiswahili zaidi kuliko lugha zingine. Mnyampala (Uk. 10)

2.2 Kaluta Amri Abedi kama mshairi
Sheikh Kaluta Amri Abedi alitumia kipaji chake cha kuimba na kughani mashairi na tenzi kuenzi matumizi ya Lugha ya Kiswahili akizidisha maneno yenye utamu wa lugha ya Kiswahili, nahau za lugha ya kiswahili .  Hali amabayo ilifanya kuwa motisha kubwa kwa wasomaji wa mashairi yake kuijua lugha na kuithamini kwa utukufu wake. Sheikh Kaluta Amri Abedi alitumia kalamu kuweka mchango wake katika kukuza lugha ya kiswahili, aliandika maandishi yanayofafanua kanuni za utungaji wa mashairi ya kiswahili,katika kitabu chake alichokiita  SHERIA ZA KUTUNGA MASHAIRI NA DIWANI YA AMRI (1953) – Katika uandishi wake alihamasisha lugha ya kiswahili Tanzania na Afrika Mashariki kwa umahiri wake:Kaluta aliwahi kutunga mashairi mbalimbali kwa lugha ya kiswahili ambapo hata alipo andika kitabu cha mashairi chenye kueleza kanuni za kutunga mashairi washairi wengiwlikipokea kwashangwe kubwa na kumsifia Rejea Almasi ya Afrika (Uk 81) ” anaeleza hiki ni kitabu  ambacho kimesadia sana kwa wale wanao taka kujifunza utunzi wa mashairi. Ni kitabu ambacho kinatumika mashuleni na hakuna mshairi wa sasa aliyeandika juu ya ushairi katika karne ya ishirini ambaye hakulazimika kumnukuu”
Kaluta akiwa na umri wa miaka 13 tu alipofiwa na baba yake aliandika ushairi wa kumwombolezea Rejerea katika Almasi ya Afrika (Uk 13-14):
Mola mrehemu baba, babaaliyenizaa,
Mola ni wewe Tawaba, mghofiri dhambi pia,
Peponi mpe maaba,na vyeo mzidishia,
Dua nitakabalia, Mola mghofiri baba,

Baba mwingi wa huruma kwa wema alinilea,
Akanitia kusoma,dini na dunia pia,
Akanifunza ya wema,ya akhera na dunia,
Dua nitakabalia Mola mghofiri baba

Baba nina mkumbuka, vile nilivyo mjua
Mkarimu hana shaka,mwenye hadhi na sitawa,
Ni mtu alotukuka,vyeo akavipandia,
Dua nitakabalia,Mola mghofiri baba
Huu ni mfano tu wa kazi ya ushairi inayoweza kuonyesha uwezo wake katika fani ya uga wa mashairi tangu akiwa mtoto mwenye umri mdogo.

 2.3 Kaluta Amri Abedi kama karii
Kaluta Amri Abedi  kwasababu ya umahiri wake katika kujishughulisha na lugha ya kiswahili na uga wa ushairi alichaguliwa kuwa Karii wa mashairi ya kiswahili (yaani msomaji, mkosoaji na mwelekezaji wa matumizi na maandishi ya lugha ya kiswahili); akiwa Karii wa Ushairi” alipokuwa  Tabora aliandika makala zake kuhusu kiswahili akasema kwa kukitukuza kiswahili huku akigusia historia yake na kukimanya kwakwe alisema: “Kwa bahati  tu nilizaliwa katika mji  ambao lugha inayosemwa ni kiswahili na utoto wangu nikasoma karibu vitabu vyote vilivyopatikana na vilivyokuwa vimeandikwa kwa lugha ya kiswahili kisha muda wote wa maisha yangu nikalazimika kukitumia kiswahili kama chombo maalumu cha kufanyia kazi nilizoshughulika nazo za semi na maandiko, ikatokea nikaanza kujali sana maneno na  nguvu yaliyo nazo, ufasaha na jinsi ya kutoa wazo lilete athari inayotakiwa, ikawa ninapoandika najitahidi kuchungua sana maneno  kuyachagua na kuyapima na kutwaa yale tu niliyo fikiri yana nguvu za kutosha kuwasilisha maoni yangu. Mnyampala (Uk46)
Kaluta alikuwa msomaji wa vitabu vya kiswahili aliweza kusoma maandishi ya waandishi wa kiswahili na alikosoa na kutoa maoni yake ili kuhakikisha kiswahili kinatumiwa kwa usahihi wake, hivyo alitumia muda wake kufuatilia maandishi na kuyafanyia marekebisho makosa ya lugha ya kiswahili katika maandishi ya waandishi.  Hali hii ilitokana na upenzi wake mkubwa kwa lugha tukufu ya kiswahili.
2.4 Kaluta Amri Abedi kama mwanaharakati
Sheikh Kaluta Amri Abedi alichochea kasi  ya matumizi ya lugha ya kiswahili, kwa madhumuni ya kutukuza lugha ya kiswahili. Mwandishi Mathias Mnyampala amemfafanua Sheikh Kaluta Amri Abedi juu ya ushupavu wake katika kutetea Misingi Imara ya Lugha ya Kiswahili. Anasema “Alikuwa hodari wa Mijadala kwa namna zote, kwenye mashindano ya dini wakati akiwa yungali kiongozi wa dini, alipambana kwa hoja na jamaa wengine katika lugha ya kiswahili kwa hoja zilizokiuka alishinda katika mambo mbalimbali mororo ya kidunia,” Pia alishinda malumbano yaliyotokea baina yake na Dkt Lyndon Harris kutokana na mashairi ya Guni hasa yaliyo ndani ya kitabu cha kilicho tafsiriwa na Mwl. Julius K. Nyerere kilicho andikwa na Shakespeare kinachoitwa Julius Kaisari .Mnyampala (Uk. 46 – 47)
           Sheikh Kaluta Amri Abedi alisisitiza zaidi lugha ya kiswahili huku akionyesha umma kwamba kiswahili ni lugha pekee inayofaa kuwa ya Taifa na Serikali, alisisitiza kuwa lugha ya kiswahili inazungumzwa na watu wengi zaidi kwa saababu imesheheni maneno mengi ya kibantu na sarufi yake ni ya kibantu hata imekuwa rahisi zaidi wananchi kujua na kujifunza kuliko lugha za kigeni.
Kwa msisitizo mkubwa Sheikh Kaluta Amri Abedi kwa kubainisha uzuri wa lugha iliyotukuka, lugha ya kiswahili alifikia kuandika maandishi ya kulikejeli kundi la watu wanaofanya juhuhudi za kujifunza lugha ya Kiingereza, Kiarabu,na Kifaransa kwamba watazijua kwa kiasi tu, hata kundi la wanaodhaniwa wana kijua kiingereza hakika yake ni kuwa hawakijui vilivyo, wakisema wanakisema cha matata matata, wakiandika pia wanaandika cha matata matata, na vyovyote vile ambavyo kujulikana kwalugha za kigeni kwa watu wengi kutakuwa kuzijua lugha hizo juu juu tu Mnyampala (Uk48).
           Ukweli Sheikh Kaluta Amri Abedi alikuwa na mapenzi ya dhati kwa lugha ya kiswahili, hata kumbukumbu yake iliyosomwa kwenye mkutano tarehe 18/01/1962 yenye kichwa “HATIMA YA KISWAHILI” iliashiria jinsi Sheikh Kaluta anavyoshika kalamu kwa makini kuweka bayana mapenzi makini kwenye lugha nzuri na makini ya kiswahili akitia motisha kwa washairi wa lugha ya kiswahili pamoja na watumiaji wa lugha ya kiswahili kuenzi, kutukuza na kuweka nia njema ya ari thabiti ya kujifunza lugha iliyotukuka  lugha ya kiswahili.Mnyampala (Uk.47).
           Sheikh Kaluta Amri Abedi alitafsiri Kurani Tukufu kwa lugha ya Kiswahili Mnyampala (Uk14).
Alipokuwa Waziri wa Sheria alitafsiri  sheria kwa lugha ya Kiswahili, hali hii ilifanya shauku ya watu kujifunza sheria kwa lugha ya Kiswahili. Mnyampala (Uk. 60).
            2.5 Kaluta Amri Abedi kama mwenyekiti wa chama cha kiswahili Afrika mashariki
Sheikh Kaluta Amri Abedi alifunguliwa wigo mpana wa kuitukuza lugha na uzuri wake pale alipoteuliwa kuwa Mwenyekiti wa Chama cha  Washairi wa Kiswahili kwa Afrika Mashariki, katika kipindi hicho Sheikh Kaluta Amri Abedi alihamasisha matumizi ya kiswahili akielezea lugha ya Kiswahili kuwa ni tunu waliyopewa kuwaunganisha, katika kipindi hicho  alishauri kiswahili kutumiwa katika elimu ya awali, kati  na vyuo vikubwa.  Kwahiyo mchango wa Kaluta Amri Abedi ni mkubwa sana katika maendeleo na ukuaji wa lugha ya kiswahili na  unafaa kuigwa na Watanzania na wana Afrika Mashariki kwa upana wa mawazo yake katika kuienzi lugha yetu ya asili Kiswahili.
                  
                 2.6 Kaluta Amri Abedi akiwa mwanasiasa
Sheikh Kaluta Amri Abed akiwa katika nyanja za siasa alitumia uwanja wa siasa katika kufanya juhudi za kuhakikisha ustawi wa lugha ya kiswahili katika matumiz, Kaluta akiwa waziri wa sheria alipiginia kiswahili kitumiwe katika shughuri za bunge, na ulisisitiza kiswahili kitumiwe katika kutafsiri sheria kuweka urahisi kwa sheria kueleweka kwa watu wote wa Tanzania ambao Lugha ya kiswahili ni lugha rahisi na yenye kueleweka kwa urahisi, Sheikh Bakri Abedi Kaluta Katika Almasi ya Afrika ameelezea katika kitabu chake kuwa akiwa waziri wa utamaduni aliendelea kupigania heshima ya kiswahili .Mara kwa mara alisisitiza juu ya umuhimu wa kutumia kiswahili katika shule zetu kuanzia shule za msingi hadi chuo kikuu.Sheikh Kaluta Amri Abedi kuonesha uzalendo katika lugha ya kiswahili aloiwahi kuwaondoa watoto wake kutoka shule ya msingi Agha Khan ambayo leo inaitwa Muhimbili, na kuwahamishia shule ya msingi ya Mnazi mmoja iliyo kuwa ikifundisha kwa kiswahili hiyo ilitokana na alipogundua watoto wake hawawezi kusoma vitabu vya dini vilivyo andikwa kwa kiswahili, Katika  (Uk 209-210). Pia Sheikh Kaluta akiwa waziri wa Utamaduni na maendeleo ya jamii aliwahi kuwa mmoja ya watu waliopendekeza kuanzishwa kwa Taasisi ya uchunguzi wa kiswahili ili iwe Taasisi yenye kusimamia matumizi ya kiswahili, Kwa mchango wake katika shughuli zake kuienzi lugha ya kiswahili Taasisi ya Ukuzaji wa Kiswahili wliamua kumtunuku cheti cha kumbukumbu ya Jubeleiya TUKI ya miaka75 tangu kuanzishwa kwake mwaka 1930-2005.

   Sheikh Kaluta Amri Abedi ametoa mchango mkubwa katika lugha ya kiswahili akiwa katika nyazifa mbalimbali kama ilivyo oneshwa kuwa alikuwa mwanaharakati wa kiswahili, Mshairi ambapo alitunga mashairi kwa kiswahili na kuimba lakini pia alikuwa mwandishi wa kitabu cha kanuni za kutunga mashairi,alikuwa mwanasiasa aliyetumia mwanvuli wa siasa kuendeleza juhudi za kuitukuza lugha ya kiswahili na kuendelea kuipigania itumike katika shughuli za bunge na pia shule za msingi, sekondari na hata vyuo vikuu,aliwahi kuwa karii na hata mwenyekiti wa chama cha mashairi Afrika mashariki.Wakati wote huu Sheikh Kaluta Amri Abedi alishadadia kiswahili kupewa kipeombele zaidi katika matumizi Tanzania na Afrika mashariki yote.Kwa kweli Sheikh Kaluta Amri Abedi ametoa mchango mkubwa katika kukua kwa lugha ya kiswahili anafaa kuigwa na kuenziwa na Watanzania na Wana Afrika mashariki kwa jumla.

MAREJELEO
Abeid, B.K.A (2010) Almasi ya Afrika- Maisha ya Sheikh Kaluta Amri Abeid 1924 – 1964.                  
                             Ahmadiyya Printing Press, Dar es Salaam.
Abidi, K.A (1954) Sheria za Kutunga Mashairi na Diwani ya Amri. East African Literature
                            Bureau.
Sambaza hii :

1 maoni:

Unknown alisema ...

Naomba kuelezwa kanuni za mashairi alizoangazia

Tafuta Kwenye Wikipedia

Matokeo ya utafutaji

 
Kwa Hisani ya : Muunda Blogu | Nawaje Ali | NAM
Fahari kwa Kiswahili Jukwaani
Hakimiliki © 2013 - 2018. Kiswahili Jukwaani - Haki Zote Zimehifadhiwa