Matini Muhimu :
Home » » Kazi Kazini ...!

Kazi Kazini ...!

Imeandikwa na; Unknown mnamo, Alhamisi, 2 Januari 2014 | Alhamisi, Januari 02, 2014



Kazi Kazini…! 
Mtoto  wangu  nampenda  sana.  Najitahidi  kumpatia  malezi  bora.  Nashughulishwa  na  chakula alacho,  maarifa  apatayo  na  tabia  akuliazo.  Kwa  kuwa  nataka  awe  bora,  namfuatilia  sana  akiwa nyumbani na zaidi awapo mazingira yaliyo mbali na nyumbani. Huko hupenda kujua yuko wapi, anafanya nini, anafanya vipi, yuko na nani katika mazingira na muda gani? Namtakia mafanikio mwanangu.  Nataka  atengenee. Naamini  kuwa  mafanikio  yake  yanategemea  sana  jitihada  za malezi  yangu  kwake. Kawaida  yangu  ni kutochelea  kilio  cha  mwana.  Haidhuru,  wakati mwingine, mtoto akililia wembe… Si kawaida  yangu kucheka na mtoto katika mazingira  yasiyo ya lazima. Hofu  yangu  ni kama  vile  kucheka  na  nyani… Najua  kuwa  tabia  hii  ya  mfumo  wa malezi  niitumiayo  na  kuikuza  kwa  mtoto  wangu  si  yenye kuridhiwa  kwake.  Natambua  shida  na usumbufu  wake.  Naamini  siku  zote  kuwa, …chumia  juani  ulie kivulini! Si  kwamba  huwezi kuchumia kivulini na kulia papo, lakini hii ni kama shabaha ya kunguru… Mimi ni mzazi. 

Wanajamii  walionizunguka  wanahitaji  maarifa.  Nipo  kwa  ajili  yao.  Jukumu  langu  ni  kutoa taaluma. Natambua  kuwa  nina  dhima  kubwa.  Nafahamu  sana  kwamba  hili  ni  jukumu zito.  Hata hivyo, najitahidi kuhakikisha kwamba jamii yangu inapata ‘elimu bora’ na kamwe si ‘bora elimu’. Elimu  kwa kujitegemea.  Elimu  kwa  kujikomboa.  Elimu  kwa  kujitambua.  Napenda  kuona wanafunzi  wangu wanaweka  kwenye  matendo  kila  dhana  mpya  wajifunzayo.  Mabadiliko  ya kiutendaji  yaonekane  kwa wanafunzi  wangu.  Thamani  ya wanafunzi  wa  elimu  ya Sekondari isilingane na ile ya wanafunzi wa elimu ya juu (Chuo). Dhamiri yangu ni kuwajengea wanafunzi wangu uwezo wa kujithamini na kuthamini uwezo wao. Wanafunzi wangu wajali wajifunzayo na wajifunzavyo. Wathamini mambo muhimu na umuhimu wa mambo hayo. Wauthamini wakati na umuhimu  wake.  Watambue  mabadiliko  ya  wakati  na  athari  za elimu  wajifunzayo  katika kupambana  na  maisha.  Ndio  maana,  sipendi  kulinyamazia  kosa  loloto (kubwa  au  dogo) lifanywalo na  (m)wanafunzi  wangu mbele  yangu  (machoni  au  kulishuhudia  katika mazingira mengine). Nipendalo  kuliona  na  ninalosisitiza  zaidi  kwa  wanafunzi  wangu  ni  kuitumia  elimu (hata iwe ya kiwango cha chini, ilimradi ni ‘elimu bora’) katika maisha ya kila siku. Mimi  ni mwalimu. 

Nimepewa kazi ya kusimamia usalama wa watembeao barabarani. Kuna watembeao kwa miguu, baiskeli, pikipiki,  gari,  n.k. Jitihada  niifanyayo  ni  kuhakikisha  kwamba  kila  mtumia  barabara hasumbuki. Sipendi kuona,  kwa  mfano,  gari  imebebeshwa  watu  (abiria)  zaidi  ya  kiwango kilichowekwa;  chombo kinatembea  mwendokasi  zaidi  ya  mwendo  unaopaswa  kulingana  na mazingira  na  wakati  kipitao chombo;  kupita sehemu  au  upande  na  mazingira  yasiyostahiki;  n.k.  Nataka  kila  mtu  awe  salama. Ndiyo  maana  kazi  yangu  inaitwa usalama  wa  raia. Kwa  jitihada zote,  napenda  kuwajibika  kwa mujibu wa  sheria. Huwa  nasimama  barabarani  kwa  muda ninaotakiwa  na  siondoki  hadi  muda  wangu  uishe. Katika  kutekeleza  majukumu  yangu,  sipendi kulifumbia macho kosa lolote (hata liwe dogo kiasi gani). Aidha, utiifu wa mtumia barabara kwa sheria  au  utaratibu  wowote  ndiyo  furaha  na  mafanikio  ya  kazi  yangu.  Mimi  ni  usalama barabarani. 

Nimekutana  na  wafanyakazi  wenzangu.  Mzazi,  mwalimu,  usalama  wa  taifa,  n.k.  Wote,  kwa nyakati  tofauti,  kutegemea jukumu  la  kila  mmoja,  wanalalamika.  Wanasema  wana  “kazi kazini…!”. Fikiria sifa zao, thamani yao na majina yao kwa jamii.  
                HAMAD, A. S. 
          0782197593 
                                                  kiswahilikwakiswahili@yahoo.com 
Sambaza hii :

0 maoni:

Tafuta Kwenye Wikipedia

Matokeo ya utafutaji

 
Kwa Hisani ya : Muunda Blogu | Nawaje Ali | NAM
Fahari kwa Kiswahili Jukwaani
Hakimiliki © 2013 - 2018. Kiswahili Jukwaani - Haki Zote Zimehifadhiwa